Jumanne, 17 Mei 2011

MKUU WA IMF ANYIMWA DHAMANA HUKO MAREKANI.

Dominique Strauss-Kahn
Mkuu wa Shirika la IMF Dominique Strauss-Kahn
Mkuu wa Shirika la fedha duniani ( IMF ) ,Dominique Strauss-Kahn, amezuiliwa katika gereza moja la wafungwa sugu ya Rikers Islands mjini New York, kwa tuhuma za kujaribu kumbaka mhudumu wa hoteli.
Jaji amesema kulikuwa na tisho la Strauss-Kahn, mwenye umri wa miaka 62, kutoroka iwapo angeachiliwa kwa dhamana. Mkurugenzi huyo alikamatwa jumamosi iliopita punde baada ya kubadili ndege. Baadaye alishtakiwa kwa kujaribu kumbaka mhudumu wa hoteli moja mjini New York.
Strauss-Kahn anakabiliwa na mashtaka saba na huenda akapewa kifungo cha hadi miaka 25 jela ikiwa atapatikana na hatia.
Mkuu huyo wa shirika la IMF amekanusha mashtaka dhidi yake.
Mawakili wake wameelezea kukasirishwa kwao baada ya kunyimwa dhamana , lakini wakasema mteja wao hatimaye ataondolewa lawama.
''Makabiliano ndiyo yameanza'', wakili wa upande wa utetezi Benjamin Brafman aliiambia mahakama.
Kutokana na kuzuiliwa kwake, Strauss-Kahn alishindwa kuhudhuria mkutano wa mawaziri wa fedha kutoka umoja wa ulaya mjini Brussels, Ubelgiji ambako mkopo wa kunusuru uchumi wa Ureno, wa kiwango cha dola milioni mia moja na kumi uliidhinishwa.
Nchi ya Ureno imekuwa ya tatu inayotumia sarafu ya Euro kupokea msaada kutoka kwa umoja wa ulaya na shirika la IMF, baada ya Ugiriki na Ireland.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni