Jumamosi, 7 Mei 2011

AL QAEDA IMETHIBITISHA KIFO CHA OSAMA KUPITIA MITANDAO YA KIJIHAD.

Al-Qaeda imethibitisha kifo cha kiongozi wake, Osama Bin Laden, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kundi hilo na kutangazwa kupitia mitandao mbalimbali ya itikadi kali.
Taarifa
Taarifa inayothibitisha kifo.

Tarifa hiyo imesema damu ya kiongozi huyo "haitapotea" na kuwa al-Qaeda itaendelea kushambulia Marekani na washirika wake.
Kifo cha Bin Laden kitakuwa "laana" kwa Marekani, na kutoa wito kwa Pakistan kuanza harakati, imesema taarifa hiyo.
Bin Laden alipigwa risasi na kufa siku ya Jumatatu, wakati makomando wa Marekani walipovamia nyumba yake katika mji wa Abbottabad nchini Pakistan.
 

Uvamizi huo ulifanywa bila ya mamlaka za Pakistan kufahamu, na hivyo kuongeza mvutano kati ya nchi hizo mbili.
Mikutano kadhaa ya hadhara ilifanyika nchini Pakistan siku ya Ijumaa, kupinga hatua hiyo.
Taarifa hiyo iliyochapishwa katika mitandao yenye itikadi kali imesema sauti ya kiongozi huyo wa al-Qaeda iliyorekodiwa wiki moja kabla ya kifo chake itatolewa hivi karibuni.
Nyumba
Makazi ya Bin Laden, Pakistan

"Damu ya Osama Bin Laden itaendelea kubaki, kwa ruhusa ya Mwenyezi Mungu, laana inayowafuata wamarekani na jamaa zao, itawafuata ndani na nje ya nchi zao," imeonya taarifa hiyo.
"Furaha yao itakuwa masikitiko, na damu yao itachanganyika na machozi. Tunatoa wito kwa Waisilamu wenzetu nchini Pakistan, ambao katika ardhi yao Sheikh Osama aliuawa, wasimame na kupambana."
Waandishi wa habari wanasema Wapakistani wengi wamekasirishwa na kile wanachoona kama Marekani kuingilia uhuru wa nchi yao.

Pia wanaishutumu serikali ya Pakistan kwa kuruhusu makomando wa Marekani kufanya shughuli zao, ingawa maafisa wanakanusha kuwa walifahamishwa.
Karibu watu 1,000 walikusanyika katikati ya mji wa Abbotabad baada ya sala ya Ijumaa, limeripoti shirika la habari la AFP.
Walichoma moto matairi ya magari, kuweka vikwazo katika barabara kuu na kupiga kelele wakisema "Hapana Marekani" na "magaidi, magaidi, Marekani ni magaidi".
Hata hivyo mwandishi wa BBC mjini Rawalpindi amesema maandamano ya kupinga Marekani yalikuwa madogo kuliko yalivyotarajiwa, huku watu 50 wakijitokeza.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni