Alhamisi, 22 Septemba 2011

WAKILI FELIX MKONGWA KIZIMBANI KWA KUGHUSHI

Wakili wa kujitegemea Felix Mkongwa amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka ya kughushi na kujipatia kiwanja kwa njia za udanganyifu.

Wakili wa Serikali Leonard Shayo alidai jana mbele ya Hakimu Mkazi Rita Tarimo kwamba Mkongwa alitenda makosa hayo Juni 3, 2005 jijini Dar es Salaam.

Katika shitaka la kwanza, anadaiwa kuwa alighushi mkataba wa kuuziana kiwanja namba 600 block G Tegeta jijini Dar es Salaam ikionesha kwamba imesainiwa na mmiliki halali George Kimwaga akijua sio kweli.

Mkongwa anadaiwa katika shitaka la pili kwamba alijipatia mali kwa njia za udanganyifu na kwamba tarehe hiyo alijipatia kiwanja hicho akionesha kwamba ameuziwa na Kimwaga.

Wakili Mkongwa amekana mashitaka hayo na yuko nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti ya dhamana yaliyomtaka kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika na kusaini hati ya dhamana ya Shilingi milioni 10. Kesi hiyo itatajwa Oktoba 24 mwaka huu.


source: http://www.wavuti.com/

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni