Alhamisi, 21 Aprili 2011

Waasi wakataa kuweka silaha chini Libya

 

Wapiganaji wa Waasi nchini Libya
Wapiganaji wa Waasi nchini Libya
Upinzani nchini Libya, umekataa pendekezo la hivi punde kutoka kwa serikali ya Kanali Muammar Gaddafi, la kuwataka kuweka silaha chini.
Msemaji wa baraza la mpito linalodhibiti mji wa Benghazi, amesema kuwa wapiganaji wa upinzani wataendelea na vita dhidi ya vikosi vya Kanali Gaddafi.
Msemaji wa kundi hilo la upinzani, Abdul Hafeel Ghoga, amewaambia waandishi wa habari kuwa Kanali Gaddafi, amependekeza mkataba huo wa kusitisha mapigano, kwa sababu wanajeshi wake wanaendelea kuangamizwa kwenye mashambulio ya anga yanayotekelezwa na wanajeshi wa NATO.
Lakini Bwana Ghoga, amesema upinzani hauwezi kusimamisha mashambulio yake dhidi ya wanajeshi wa serikali.
Akizungumzia pendekezo la kuafikiwa kwa mkataba wa kisiasa ambao utaruhusu kiongozi wa Libya, Kanali Gaddafi na familia yake kusalia nchini humo, Ghoga amesema hilo haliwezekani.
Msemaji huyo wa upinzani amesema, kwa sasa hakuna mzozo wa kijeshi nchini humo.
Amesema kuongezwa kwa mashambulio ya anga yanayofanywa na wanajeshi wa NATO, kumeimarisha hali kwa waasi wanaopinga serikali ya Gadaffi.
Huku hayo yakijri, mtengenezaji filamu mmoja aliyeteuliwa kuwania tuzo la filamu maarufu kama Oscars, ameuawa mjini Misrata.
Tim Hetherington
Tim Hetherington
Tim Hetherington, ambaye ana uraia wa Uingereza na Marekani aliuawa kwenye shambulio kati kati mwa mji huo ambao umeendelea kushuhudia mapigano makali kati ya wanajeshi watiifu kwa Kanali Gaddafi na wale wa waasi.
Hetherington alikuwa mmoja wa wasimamzi wa filamu ya Resrepo iliyotengenezwa kuhusu vita vya Afghanistan.
Filamu hiyo iliteuliwa kuwania tuzo la oscar mwaka huu.
Mwandishi mwingine Chris Hondros, raia wa Marekani ambaye alikuwa miongoni mwa waliojeruhiwa kwenye shambulio hilo, aliaga dunia akipokea matibabu hospitalini.
Ripoti zinasema mwandishi mwingine wa habari pia alijeruhiwa kwenye shambulizi hilo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni