Ijumaa, 18 Mei 2012

RUNGU LA CAG LAWAANGUKIA WATUMISHI WA HALMASHAURI YA WILAYA YA SONGEA.

RUNGU la mkaguzi na mdhibiti wa hesabu za serikali (CAG) Ludovick Utouh, limetua Songea ambako baraza la madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma limewasimamisha kazi watendaji wanne wa idara ya uhasibu akiwemo mweka hazina wa halmashauri ya jiji la Tanga Anna Mbogo, ambaye alikuwa kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo kabla ya kuhamishiwa Tanga. Watendaji hao ambao wanadaiwa kuwa ndio waliosababisha halmashauri hiyo kupata hati chafu.
Jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Songea almaarufu Jumba la Maendeleo, vikao vya Baraza la madiwani hufanyika hapa.
Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Songea Rajabu Mtyula aliwataja watendaji wengine waliosimamishwa kazi kuwa ni Elems Salvatory ambaye ni kaimu mweka hazina, mhasibu wa mapato Joseph Mazito na Elishiria Mnzava ambaye ni mkaguzi wa mahesabu ya ndani.

Mtyula alisema kuwa halmashauri yake imeamua kutoa maamuzi magumu kwa watendaji hao ambao ndio waliosababisha halmashauri hiyo iwe miongoni mwa halmashauri tano zilizopata hati chafu hapa nchini. Ambapo alibainisha zaidi kuwa taarifa zisizo sahihi kwenye taarifa ya mtiririko wa fedha kuwa taarifa ya zidio la uchakavu wa mali zisizodhahiri za ruzuku ya maendeleo kwa sh.13, 167,862,807/=.

Alifafanua zaidi kuwa uhamisho wa ndani wa fedha kiasi cha sh. 12,854,970,498/= uliingizwa katika taarifa ya mtiririko wa fedha kama mapokezi ya fedha taslimu, kushuka kwa wadaiwa kulitolewa taarifa zaidi kiasi cha sh. 39,124,400/= na kuongezeka kwa wadai kulitolewa zaidi kwa sh. 14,226,587/=

Alisema kuwa hati za malipo zenye jumla ya sh. 15,315,467/= hazikuwakilishwa kwa ukaguzi, mapato yenye jumla ya sh. 913,000/= yalikusanywa lakini hayakuwasilishwa kwa mtunza fedha wa halmashauri, kuwepo malipo yasiyo na viambatanisho sahihi ya thamani ya sh. 56,690,784.38/= na vitabu vitano vya mapato halmashauri hiyo havikuwakilishwa kwa mkaguzi jambo ambalo lilionesha wazi kuwa kuna ubadhirifu mkubwa wa fedha ndani ya halmashauri hiyo.

Mtyula ambaye pia ni diwani wa kata ya Mpitimbi, alisema kuwa makosa hayo ndiyo yaliyosababishwa na utendaji mbovu wa idara ya fedha kupitia kwa wataalamu waliofanya kazi ya kufunga hesabu za halmashauri hiyo waliokuwa wanaongozwa na aliyekuwa kaimu mkurugenzi kwa wakati huo Anna Mbogo ambapo kwa sasa amehamishiwa katika halmashauri ya jiji la Tanga kama mweka hazina.

Alisema kuwa halmashauri yake  baada ya kupokea taarifa hiyo iliitisha kikao maalumu Mei 12 mwaka huu ili kujadili kwa kina majibu ya hoja zote zilizoletwa na wataalamu kutoka CAG pia serikali kupitia wizara ya tawala za mikoa na serikali za mitaa imetoa waraka kwa barua ya Mei 14 mwaka huu wa maelekezo ya namna ya kuwashughulikia na kuwachukulia hatua za kinidhamu na kisheria haraka sana wale wote waliohusika kupatikana kwa hati chafu.

Kutokana na hali hiyo madiwani wa halmashauri hiyo kwa pamoja wameadhimia kuwasimamisha kazi watendaji wanne wa hamshauri hiyo na kuvitaka vyombo vingine kikiwemo chombo cha dola kuona ni namna gani watendaji hao watawajibishwa ilikulinda heshima ya halmashauri.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni