Jumapili, 29 Aprili 2012

JOHN KOMANYA, ASKOFU ANYEDAIWA KUWATAPELI WAUMINI.

ASKOFU wa Kanisa la Cathedral of Joy International Tanzania, John Komanya anadaiwa kutapeli waumini wake Sh milioni 12.5 katika matukio tofauti.
 Image
Askofu Komanya.

Mmoja wa wanaodaiwa kutapeliwa, Allen Mishili amesema juhudi za kudai fedha hizo zimeshindikana na hivyo wametoa taarifa Polisi na kufungua jalada namba DSM/KIN/OD/PE 36/2012, Machi mosi.
Akisimulia tukio hilo kwa kina, Mishili alidai kuwa Agosti mwaka jana kupitia Wapo Radio alimsikia Askofu Komanya akitoa maono yake yakifanana na maisha ya familia yake, akisema Mungu amemtuma kumponya mama yake ambaye alikuwa mgonjwa.

“Maelezo aliyoyatoa yaliilenga familia yangu kabisa, alieleza kuhusu wazazi wangu na jinsi
mama yangu anavyoumwa, nami niliwajulisha watu wa familia yangu, ili tumtafute kwa njia ya
simu na akanitaka nifike Legho, Sinza, Kinondoni liliko kanisa lake.

“Jumapili nilikwenda kanisani na kukaa kiti cha mwisho kabisa, baada ya ibada nilikwenda kujitambulisha nikapewa Mchungaji Togolani Mnkande na kwenda naye hospitali ya Mama Ngoma, ambako alimwombea mgonjwa na kumfanyisha mazoezi. Kesho yake, mke wangu (Getrude) pia alikwenda kuombewa baada ya kutojisikia vizuri,” alidai Mishili.

Aliendelea kudai kwamba katika jambo la kushangaza, ndani ya wiki moja tayari alishawachagua kuwa miongoni mwa viongozi wa Kanisa na kushiriki vikao vya kuimarisha
Kanisa ikiwa ni kutimiza alichodai Askofu Komanya kutumwa na Mungu.

“Jumatano alinipa nafasi ya kuongoza Kanisa, Ijumaa nikaongoza mkesha. Alitwambia ametoka Marekani baada ya kutumwa na Mungu, ili kuwatapisha watu ‘kikombe cha babu’.

Lakini sasa tumebaini kuwa alikuwa nchini tangu Aprili mwaka jana.” Mishili aliongeza: “Tukiwa tunaelekea wiki ya pili, alitufuata na kututaka tumtengenezee kitanda, kwani kwa wakati huo alidai hataki kuishi hotelini na kuwa Kanisa lilikuwa limempangishia nyumba Kimara.Thamani ya kitanda, godoro na feni ilikuwa ni Sh 1, 850, 000 ambazo aliahidi kulipa.”

Alidai kuwa walipeleka kitanda hicho Kimara kwenye nyumba ambayo ilikuwa haikaliwi na mtu zaidi ya muumini wa Kanisa hilo aliyetajwa kwa jina moja la Fredy.

“Tuliamini tutalipwa, kwani ni mtumishi wa Mungu, baada ya wiki nne bila kulipwa Askofu Komanya alitangazia waumini kuwa kitanda anacholalia bado hakijalipwa, hivyo alitaka
wachangishe fedha hizo,” alidai Mishili.

Ndani ya mwezi mmoja, wakiwa kwenye vikao alitaka akopeshwe Sh milioni 2 za kugharimia kikundi cha kwaya cha Kanisa hilo ambacho alikiweka kambini Bagamoyo kujiandaa na Mkutano wa Injili aliopanga kuufanya Morogoro.

“Alitaka kukopa kwa riba, kwa sababu sisi ni wafanyabiashara, tulikwenda kwa mtu anayekopesha ambaye alitaka alipwe asilimia 15, akaahidi kuzilipa ndani ya siku tatu; tukamshauri kulipa ndani ya wiki moja. Fedha hizo tulizituma kwa M-Pesa kwenda Bagamoyo, nazo hazijalipwa na zimetuletea matatizo makubwa na kutuvunjia uaminifu.”



Mishili alidai kuwa kana kwamba haitoshi, Askofu Komanya aliibuka tena na kudai mkopo wa Sh milioni saba za kukombolea gari lake aina ya Ford aliloweka rehani kwa mtu Kurasini, Dar es Salaam, ambazo alidai angezilipa baada ya kuuza gari hilo kwa Sh milioni 23.

“Tulimpa fedha hizo mbele ya dada yake (jina tunalo) ambaye alikuwa Mweka Hazina wa
Kanisa na kubwa zaidi alituahidi kuwa wakati gari linasubiri kuuzwa tutaliegesha nyumbani
kwetu mpaka hapo fedha zitakaporejeshwa, lakini haikuwa hivyo.”

Mishili alidai kuwa Askofu Komanya kwa mara nyingine alitaka mkopo wa Sh 200,000 ambazo
angelipa baada ya Ibada na aliagiza apewe kijana aliyemtaja kwa jina moja la Dereck, baada ya
kifaa cha umeme kuharibika kwenye vyombo vya muziki.

“Kusema ukweli katika miezi miwili, kwa maelezo tofauti alichukua hizo fedha na hakuna hata senti moja aliyorudisha, na baya zaidi alitutenganisha na familia maana alisema mama yangu
(ambaye ni marehemu sasa) alikuwa mchawi na ndiye aliyefanya mke wangu asizae,”
alilalamika Mishili.

Aliongeza: “Tulikuwa na deni benki, akatwambia Mungu amemwonesha kuwa deni hilo
litakwisha, kumbe alikwenda kwa baba na kumlazimisha kulilipa, baba hakupenda hali hiyo na
pamoja na maneno machafu aliyosema dhidi ya mama hospitalini kwa Mama Ngoma,
tulitengwa na familia.”

Baada ya kubaini kuwa Askofu Komanya hana Nguvu za Mungu kama alivyotamba na anatapeli, walirejea kwenye Kanisa lao la Ufufuo na Uzima na kudai fedha zao ambazo Askofu Komanya alikataa kulipa kwa anachodai kuwa ni zaka.

“Baada ya kubaini kuwa maono anayodai kuwa ni ya Mungu hayana ukweli, tulitengana naye na kudai fedha zetu, mwanzo alitutumia ujumbe mfupi na akitwambia angetulipa Novemba 20 mwaka jana, lakini baadaye akaanza kututumia ujumbe wa vitisho.

“Alituambia twende tutakako na hawezi kufanywa kitu chochote, Rais Jakaya Kikwete ni mtu
wake na pia yeye ni Ofisa Usalama wa Kikosi cha Mbwa. Hata hivyo sisi tunaamini vyombo vya
Dola vitatetea haki yetu.

Gazeti hili lilipata nakala ya barua ya Kanisa la Cathedral of Joy International Tanzania lenye
usajili namba S.A 17058 (CAP 337 R.E 2002) ya Machi 9 mwaka huu iliyosainiwa na Katibu Mtendaji wake, Majili Stephen Killo, akikiri kutambua kudaiwa kiasi hicho cha fedha.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela, alikiri kufunguliwa kwa jalada
hilo dhidi ya Askofu Komanya kuhusu tuhuma hizo za utapeli.

“Ni kweli Askofu huyo amefunguliwa jalada na mama anayedai kutapeliwa Sh milioni 12.5 na Askofu huyo,” alisema.

Kamanda Kenyela alisema kwa kumbukumbu za kipolisi, Askofu huyo pia alipata kufunguliwa malalamiko kama hayo Sombetini, Arusha, akidaiwa kumtapeli mtu Sh milioni mbili na kusisitiza kwamba mambo yote hayo yanachunguzwa na baadaye itafahamika ni hatua gani
zichukuliwe.

Alipoulizwa, mmoja wa viongozi wa Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania, Mtume
Onesmo Ndege, alikubali kupokea malalamiko hayo na kwamba alifanya juhudi za kuwasiliana na Askofu Komanya ili kujua kiini cha tatizo, lakini hakutokea.

“Nimemwambia kwa kukataa mwito wangu atalazimika kubeba matokeo ya kile nilichomwitia.
Nililetewa malalamiko kama mimi na nikaona niyashughulikie, kwa sababu siku moja Askofu Komanya aliniomba niwe baba yake wa kiroho, lakini nilikataa kutokana na kutojua mienendo
yake,” alisema

Maoni 5 :

  1. kwa muda mrefu nimekuwa nikisikia scandal za huyu Askofu,kuanzia akiwa Mwanza,sasa inaenda kuthibitisha ya kwamba lisemalo lipo,anatuhuma si tu za fedha bali za ngono pia.

    JibuFuta
  2. Nina information za uhakika toka kwa aliyewahi kuwa mchungaji wake Mwanza,akaondoka kutokana na kusimamia ukweli wa tuhuma za uzinzi wa huyu Askofu,

    JibuFuta
  3. Eti inasemekana ni Mfanyakazi wa Idara ya Usalama wa Taifa huko Ikulu ya Dar es Salaam, kuna ukweli wowote!!!!? Maana asije uza nchi huyu inaonekana ana tamaa sana.

    JibuFuta
  4. ni kweli kabisa huyo mtu ni mzinzi na tapeli wa kufa mtu, hana nguvu ya mungu hata kidogo. hafai kabisa.

    JibuFuta
  5. huyu mtu sio mtumishi wa serikali hata kidogo.kama kuna mtu anaweza kuthibitisha maneno ya john atuambie au afike ofisi za serikali atusaidie tukomeshe hilo.nikosa la jinai mtu kujifanta mtumishi wa serikali

    JibuFuta