Jumapili, 2 Septemba 2012

RAIS KIKWETE AFAFANUA JUU YA MGOGORO WA MPAKA WA MALAWI NA TANZANIA.

Rais Jakaya Kikwete
Tausi Mbowe
RAIS Jakaya Mrisho Kikwete, amesema kuwa mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa baina ya Tanzania na Malawi, utamalizwa kwa mazungumzo huku akisema chimbuko la mzozo huo ni mkataba wa Heligoland uliowekwa na wakoloni .

Akihutubia taifa kupitia hotuba yake ya kila mwezi, Rais Kikwete alisema kuwa siyo makusudio yake, wala ya Serikali kutafuta suluhisho la suala hilo kwa nguvu za kijeshi.

“Nawahakikishia Watanzania wenzangu kuwa, hatuko vitani na Malawi na wala hakuna maandalizi ya vita dhidi ya jirani zetu hawa kwa sababu ya mzozo wetu wa mpaka katika ziwa...  Ondoeni hofu na endeleeni na shughuli zenu za ujenzi wa taifa letu kama kawaida, ” alisisitiza Rais Kikwete.

Alisema kuwa alipokutana na Rais wa Malawi, Joyce Banda mjini Maputo, Msumbiji Agosti 18, 2012 alimhakikishia kuwa Tanzania haina mpango wa kuingia vitani na Malawi.

Rais Kikwete aliwataka wanasiasa kuepuka kauli au matendo yatakayovuruga mazungumzo na kuchochea uhasama kati ya nchi hizo mbili jirani na rafiki, huku akisisitiza kuwa kuna mafanikio makubwa ya kumaliza mzozo huo kwa njia ya mazungumzo kuliko njia ya vita, kwa kuwa kwa kufanya hivyo badala ya kupata suluhisho inaweza kuwa ndiyo mwanzo wa mgogoro mpana zaidi.

Alisema utata kuhusu mpaka katika Ziwa Nyasa haukuanza leo na kwamba ulikuwapo tangu wakati nchi hizo mbili zikiwa bado zinatawaliwa na wakoloni na kuendelea hata baada ya uhuru.

Chimbuko la mzozo
Rais Kikwete alisema chimbuko la mzozo wa mpaka uliopo sasa, baina ya nchi hizo mbili ni makubaliano baina ya Waingereza na Wajerumani kuhusu mpaka baina ya nchi hizo yaliyofanywa Julai Mosi, 1890, ambayo yalijulikana kama Mkataba wa Heligoland, (The Anglo-Germany Heligoland Treaty) ambayo yalitiwa saini Berlin, nchini Ujerumani baina ya Waingereza na Wajerumani.

Alisema wakoloni hao walikubaliana kuhusu mipaka baina ya makoloni yao na wakoloni wengine waliopakana nao, ambapo ndiyo makubaliano yaliyoweka mipaka ya Tanganyika na ile ya Zanzibar .

Rais Kikwete alisema kuwa kwa upande wa Ziwa Nyasa, Waingereza na Wajerumani walikubaliana kuwa mpaka uwe kwenye ufukwe wa nchi ya Tanzania kwa maana hiyo ziwa lote likapewa nchi ya Malawi na kwa upande wa Mto Songwe mpaka ulikuwa ufukweni upande wa Malawi kwa maana hiyo mto wote ukawa upande wa Tanzania.

Alisema katika kipengele cha Sita (Article VI) cha mkataba huo, wakoloni hao walikubaliana kufanya marekebisho ya mpaka mahali popote kama itakuwa ni lazima kufanya hivyo, kulingana na mazingira na hali halisi ya mahali hapo.

Alisema mwaka 1898 Tume ya Mipaka iliundwa na kuanza  kazi katika Mto Songwe kuhakiki mpaka baina ya Tanzania  na Malawi, ambapo ilikubaliana kuhamisha mpaka kutoka ufukweni mwa Mto Songwe upande wa Malawi na kuwa katikati ya mto.

“Baada ya uhakiki katika eneo hilo kukamilika, mwaka 1901 mkataba mpya ulisainiwa kuhusu mpaka huo...Tume iliendelea na kazi yake katika Ziwa Tanganyika na kuhamisha mpaka kutoka ufukweni hadi katikati ya ziwa na mkataba mpya kusainiwa mwaka 1910,” alisema.

Rais Kikwete alisema bahati mbaya tume hiyo haikufanikiwa kufanya uhakiki wa mpaka katika Ziwa Nyasa kutokana na kutokea kwa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia kati ya mwaka 1914 hadi 1918 ambapo baada ya vita hivyo na Ujerumani kushindwa, Baraza la Umoja wa Mataifa liliikabidhi Uingereza udhamini wa Tanganyika na kwamba Uingereza ikawa inatawala Malawi na Tanganyika.

Alisema wakati Tume ya Uingereza na Ujerumani ilipokuwa imekufa, Tume ya Mipaka kati ya Uingereza na Ureno iliendelea na kazi na matokeo yake mwaka 1954, Uingereza na Ureno zilitengua mkataba wao wa mwaka 1891 ulioweka mpaka wa Ziwa Nyasa katika ufukwe wa mashariki ya ziwa, yaani kwenye ufukwe wa Msumbiji na kuuhamishia katikati ya ziwa.

Alisema jambo la kustaajabisha ni kuwa, Waingereza walioona umuhimu na busara ya kurekebisha mpaka kati ya Malawi na Msumbiji, hawakuona umuhimu wa kufanya hivyo kati ya nchi ya Tanzania na Malawi licha ya watu kutaka ufafanuzi kwa sababu inasemekana kati ya mwaka 1925 na 1938, taarifa ya Uingereza kwa Umoja wa Mataifa ziliweka mpaka katikati ya ziwa.  Lakini, kuanzia mwaka 1948 mpaka ukawekwa tena ufukweni.

“Mwaka 1959, 1960 na 1962, suala la mpaka wa Malawi lilijitokeza tena na kujadiliwa na Bunge la Tanganyika, wakati ule lilijulikana kuwa Baraza la Kutunga Sheria, (Legislative Council – LEGCO)," alisema.

Alisema hoja iliyotolewa ilikuwa kwamba Serikali ya Tanganyika ijadiliane na Serikali ya Nyasaland kupitia Serikali ya Malkia wa Uingereza ili ufumbuzi upatikane.  Wakoloni hawakujali na wala hakuna hatua zilizochukuliwa mpaka Tanganyika ikapata uhuru wake Desemba 9, 1961 na Malawi kupata uhuru wake mwaka 1964.”

Rais Kikwete aliongeza kuwa, wakati Tanzania ilipopata uhuru mwaka 1961, mjadala kuhusu mpaka wa Tanganyika na Malawi uliendelea bungeni, hata hivyo iliamuliwa kwamba isubiriwe mpaka Malawi wapate uhuru ili yafanyike mazungumzo baina ya nchi mbili huru.

Alisema kuwa tangu wakati huo Tanzania haikukata tamaa katika awamu zote za uongozi imekuwa ikijitahidi kuendelea na jitihada za kumaliza mgogoro huo.

Kikwete alisema tume ya sasa itatoa mapendekezo kwa marais wa nchi hizo mbili, ambayo yatakuwa msingi wa majadiliano baina yao.  Alisisitiza umuhimu wa kulipatia ufumbuzi suala hilo.

Sensa
Akizungumza kuhusu zoezi la Sensa ya Watu na Makazi, Rais Kikwete alisema mpaka sasa mwelekeo ni mzuri na ugumu ulioonekana kuwepo pale mwanzoni uliendelea kupungua siku hadi siku kadri utekelezaji wa zoezi ulivyokuwa unaendelea hivyo ana matumaini makubwa kuwa Sensa ya mwaka huu itakuwa na mafanikio mazuri.

Alitoa wito kwa wale wote ambao hawajahesabiwa wafanye hivyo katika siku zilizoongezwa ikiwa ni pamoja na wao wenyewe kupeleka taarifa zao kwa wenyeviti wao wa Serikali za mitaa au vijiji.

Alisema amearifiwa kwamba kama mambo yatakwenda kama ilivyopangwa, matokeo ya awali ya Sensa ya Watu na Makazi kuhusu idadi ya watu na jinsia zao yatatolewa mwishoni mwa mwaka huu

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni